Psalms 80
Maombi Kwa Ajili Ya Kuponywa Kwa Taifa
Kwa mwimbishaji. Mtindo wa “Yungiyungi za Agano.” Zaburi ya Asafu. 1Ee Mchungaji wa Israeli tusikie,wewe umwongozaye Yosefu kama kundi;
wewe uketiye katika kiti cha enzi
katikati ya makerubi, angaza
2mbele ya Efraimu, Benyamini na Manase.
Uamshe nguvu zako,
uje utuokoe.
3Ee Mungu, uturejeshe,
utuangazie uso wako,
ili tuweze kuokolewa.
4Ee Bwana Mungu Mwenye Nguvu Zote,
hata lini hasira yako itawaka na kufoka moshi
dhidi ya maombi ya watu wako?
5Umewalisha kwa mkate wa machozi,
umewafanya wanywe machozi bakuli tele.
6Tumekuwa chanzo cha ugomvi kwa jirani zetu,
na adui zetu wanatudhihaki.
7Ee Mungu Mwenye Nguvu Zote, uturejeshe;
utuangazie uso wako,
nasi tuweze kuokolewa.
8Ulileta mzabibu kutoka Misri,
ukawafukuza mataifa, ukaupanda.
9Uliandaa shamba kwa ajili yake,
mizizi ikawa imara, ukajaza nchi.
10Milima ilifunikwa kwa kivuli chake,
matawi yake yakafunika mierezi mikubwa.
11Matawi yake yalienea mpaka Baharini, ▼
▼Huenda inamaanisha Bahari ya Mediterania.
machipukizi yake mpaka kwenye Mto. ▼
▼Yaani Mto Frati.
12Mbona umebomoa kuta zake
ili wote wapitao karibu
wazichume zabibu zake?
13Nguruwe mwitu wanauharibu
na wanyama wa kondeni hujilisha humo.
14Turudie, Ee Mungu Mwenye Nguvu Zote!
Tazama chini kutoka mbinguni na uone!
Linda mzabibu huu,
15mche ulioupanda kwa mkono wako wa kuume,
mwana uliyemlea
kwa ajili yako mwenyewe.
16Mzabibu wako umekatwa, umechomwa moto,
unapowakemea, watu wako huangamia.
17Mkono wako na utulie juu ya mtu aliyeko mkono wako wa kuume,
mwana wa mtu uliyemlea kwa ajili yako mwenyewe.
18Ndipo hatutakuacha tena,
utuhuishe, nasi tutaliitia jina lako.
19Ee Bwana Mungu Mwenye Nguvu Zote, uturejeshe;
utuangazie uso wako,
ili tuweze kuokolewa.
Copyright information for
SwhNeno