‏ Psalms 146

Kumsifu Mungu Mwokozi

1Msifuni Bwana!
Msifuni Bwana kwa Kiebrania ni Hallelu Yah.

Ee nafsi yangu, umsifu Bwana,
2Nitamsifu Bwana maisha yangu yote;
nitamwimbia Mungu wangu sifa
wakati wote niishipo.
3Usiweke tumaini lako kwa wakuu,
kwa wanadamu ambao hufa,
ambao hawawezi kuokoa.
4Roho yao itokapo hurudi mavumbini,
siku hiyo hiyo mipango yao yote hukoma.

5Heri yeye ambaye Mungu wa Yakobo ni msaada wake,
ambaye tumaini lake ni katika Bwana, Mungu wake,
6Muumba wa mbingu na nchi,
na bahari na vyote vilivyomo ndani yake:
Bwana anayedumu kuwa mwaminifu
milele na milele.
7Naye huwapatia haki walioonewa
na kuwapa wenye njaa chakula.
Bwana huwaweka wafungwa huru,
8 Bwana huwafumbua vipofu macho,
Bwana huwainua waliolemewa na mizigo yao,
Bwana huwapenda wenye haki.
9 Bwana huwalinda wageni
na kuwategemeza yatima na wajane,
lakini hupinga njia za waovu.

10 Bwana atamiliki milele,
Mungu wako, ee Sayuni,
kwa vizazi vyote.

Msifuni Bwana.
Copyright information for SwhNeno