‏ Psalms 62

Mungu Kimbilio La Pekee

Kwa mwimbishaji. Mtindo wa Yeduthuni. Zaburi ya Daudi.

1Kwa Mungu peke yake nafsi yangu inapata pumziko;
wokovu wangu watoka kwake.
2Yeye peke yake ndiye mwamba wangu na wokovu wangu;
yeye ni ngome yangu, sitatikisika kamwe.

3Mtamshambulia mtu hata lini?
Je, ninyi nyote mtamtupa chini,
ukuta huu ulioinama na uzio huu unaotikisika?
4Walikusudia kikamilifu kumwangusha
toka mahali pake pa fahari;
wanafurahia uongo.
Kwa vinywa vyao hubariki,
lakini ndani ya mioyo yao hulaani.

5Ee nafsi yangu, upumzike, kwa Mungu peke yake,
tumaini langu latoka kwake.
6Yeye peke yake ndiye mwamba wangu na wokovu wangu;
ndiye ngome yangu, sitatikisika.
7Wokovu wangu na heshima yangu viko kwa Mungu,
ndiye mwamba wangu wenye nguvu
na kimbilio langu.
8Enyi watu, mtumainini yeye wakati wote,
miminieni mioyo yenu kwake,
kwa kuwa Mungu ni kimbilio letu.

9Binadamu wa ngazi ya chini ni pumzi tu,
nao wa ngazi ya juu ni uongo tu;
wakipimwa kwenye mizani, si chochote;
wote kwa pamoja ni pumzi tu.
10Usitumainie vya udhalimu
wala usijivune kwa vitu vya wizi;
ingawa utajiri wako utaongezeka,
usiviwekee moyo wako.

11Jambo moja Mungu amelisema,
mambo mawili nimeyasikia:
kwamba, Ee Mungu,
wewe una nguvu,
12na kwamba, Ee Bwana,
wewe ni mwenye upendo.
Hakika utampa kila mtu thawabu
kwa kadiri ya alivyotenda.
Copyright information for SwhNeno