‏ Psalms 83

Maombi Kwa Ajili Ya Kushindwa Kwa Adui Wa Israeli

Wimbo. Zaburi ya Asafu.

1Ee Mungu, usinyamaze kimya,
usinyamaze, Ee Mungu, usitulie.
2Tazama watesi wako wanafanya fujo,
jinsi adui zako wanavyoinua vichwa vyao.
3Kwa hila, wanafanya shauri dhidi ya watu wako,
wanafanya shauri baya dhidi ya wale unaowapenda.
4Wanasema, “Njooni, tuwaangamize kama taifa,
ili jina la Israeli lisikumbukwe tena.”

5Kwa nia moja wanapanga mashauri mabaya pamoja,
wanafanya muungano dhidi yako,
6mahema ya Edomu na Waishmaeli,
ya Wamoabu na Wahagari,
7Gebali,
Yaani Bubilo, mji wa zamani sana wa Ufoinike (kama kilomita 80 kaskazini mwa Beiruti).
Amoni na Amaleki,
Ufilisti, pamoja na watu wa Tiro.
8Hata Ashuru wameungana nao
kuwapa nguvu wazao wa Loti.

9Uwatendee kama vile ulivyowatendea Midiani,
na kama vile ulivyowatendea Sisera na Yabini
hapo kijito cha Kishoni,
10ambao waliangamia huko Endori
na wakawa kama takataka juu ya nchi.
11Wafanye wakuu wao kama Orebu na Zeebu,
watawala wao kama Zeba na Salmuna,
12ambao walisema, “Na tumiliki nchi
ya malisho ya Mungu.”

13Ee Mungu wangu, wapeperushe kama mavumbi ya kisulisuli,
kama makapi yapeperushwayo na upepo.
14Kama vile moto uteketezavyo msitu
au mwali wa moto unavyounguza milima,
15wafuatilie kwa tufani yako
na kuwafadhaisha kwa dhoruba yako.
16Funika nyuso zao kwa aibu
ili watu walitafute jina lako, Ee Bwana.

17Wao na waaibishwe na kufadhaishwa milele,
na waangamie kwa aibu.
18Hebu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Bwana,
kwamba wewe peke yako ndiwe Uliye Juu Sana ya dunia yote.
Copyright information for SwhNeno