‏ Deuteronomy 14:3-21

3Msile kitu chochote ambacho ni machukizo. 4Hawa ndio wanyama mtakaokula: ngʼombe, kondoo, mbuzi, 5kulungu, paa, kongoni, paa mweupe, mbuzi-mwitu, pofu na kondoo wa mlimani. 6Mnaweza kumla mnyama yeyote mwenye kwato zilizogawanyika mara mbili, pia yule anayecheua. 7Hata hivyo, miongoni mwa wale wanaocheua au wale walio na kwato zilizogawanyika kamwe msile ngamia, sungura na pelele. Iwapo wanacheua, lakini hawana kwato zilizogawanyika; ni najisi kwenu kwa taratibu za kiibada. 8Nguruwe pia ni najisi; ingawa ana kwato zilizogawanyika, hacheui. Msile nyama yake wala kugusa mzoga wake.

9Katika viumbe hai vyote viishivyo kwenye maji, mnaweza kula yeyote aliye na mapezi na magamba. 10Lakini chochote kisicho na mapezi na magamba msile; kwenu ni najisi.

11Mnaweza kula ndege yeyote aliye safi. 12Lakini wafuatao msiwale: tai, furukombe, kipungu, 13kengewa mwekundu, kengewa mweusi, mwewe wa aina yoyote, 14kunguru wa aina yoyote, 15mbuni, kiruka-njia, dudumizi, kipanga wa aina yoyote, 16bundi, mumbi, bundi mkubwa, 17mwari, nderi, mnandi, 18korongo, koikoi wa aina yoyote, hudihudi na popo.

19Wadudu wote warukao kwa makundi ni najisi kwenu, msiwale. 20Lakini viumbe vyote vyenye mabawa vilivyo safi mwaweza kula.

21Msile kitu chochote mtakachokuta kimekufa. Mnaweza kumpa mgeni yeyote anayeishi katika mojawapo ya miji yenu, naye anaweza kula au mnaweza kumuuzia mtu wa nchi nyingine. Lakini ninyi ni watu watakatifu kwa Bwana Mungu wenu.

Msitokose mwana-mbuzi katika maziwa ya mama yake.
Copyright information for SwhNeno