Exodus 39:22-31
Mavazi Mengine Ya Kikuhani
(Kutoka 28:31-43)
22Akashona joho la kisibau lote kwa kitambaa cha rangi ya buluu tupu, kazi ya mfumaji, 23na lilikuwa na nafasi ya shingo katikati ya joho lile iliyofanana na ukosi, na utepe ulioshonwa kuizunguka nafasi hiyo ili isichanike. 24Akatengeneza makomamanga ya nyuzi za rangi ya buluu, za zambarau, na nyekundu na ya kitani iliyosokotwa vizuri kuzunguka pindo la hilo joho. 25Kisha akatengeneza vikengele vya dhahabu safi na kuvishikamanisha kuzunguka pindo hilo kati ya hayo makomamanga. 26Hivyo vikengele na makomamanga vilipishana kuzunguka upindo wa joho ili livaliwe kwa kuhudumu, kama Bwana alivyomwagiza Mose. 27Pia akamtengenezea Aroni na wanawe makoti ya kitani safi, kazi ya mfumaji, 28na kilemba cha kitani safi, tepe za kichwani za kitani, na nguo za ndani za kitani iliyosokotwa vizuri. 29Mshipi ulikuwa wa kitani iliyosokotwa vizuri ya rangi ya buluu, na zambarau, na nyekundu, kazi ya mtarizi, kama Bwana alivyomwagiza Mose. 30Kisha akatengeneza lile bamba, taji takatifu, kwa dhahabu safi na kuchora juu yake maneno haya kama vile muhuri huchorwa: Mtakatifu kwa Bwana. 31Kisha wakalifunga kwa kamba ya rangi ya buluu ili kulishikamanisha na kile kilemba kama Bwana alivyomwagiza Mose.
Copyright information for
SwhNeno