Mark 3:20-30
Yesu Na Beelzebuli
(Mathayo 12:22-32; Luka 11:14-23; 12:10)
20Kisha Yesu aliporudi nyumbani, umati wa watu ukakusanyika tena, kiasi kwamba yeye na wanafunzi wake hawakuweza kula chakula. 21Ndugu zake walipopata habari wakaja ili kumchukua kwa maana watu walikuwa wakisema, “Amerukwa na akili.” 22Walimu wa sheria walioteremka kutoka Yerusalemu walisema, “Amepagawa na Beelzebuli! ▼▼Beelzebuli kwa Kiyunani ni Beelzebubu, yaani mkuu wa pepo wachafu.
Anatoa pepo wachafu kwa kutumia mkuu wa pepo wachafu!” 23Basi Yesu akawaita na kuzungumza nao kwa mifano akasema: “Shetani awezaje kumtoa Shetani? 24Kama ufalme ukigawanyika dhidi yake wenyewe, ufalme huo hauwezi kusimama. 25Nayo nyumba kama ikigawanyika dhidi yake yenyewe, nyumba hiyo haiwezi kusimama. 26Naye Shetani kama akijipinga mwenyewe na awe amegawanyika, hawezi kusimama bali mwisho wake umewadia. 27Hakuna mtu yeyote awezaye kuingia kwenye nyumba ya mtu mwenye nguvu na kuteka nyara mali zake asipomfunga kwanza yule mwenye nguvu. Ndipo ataweza kuteka nyara mali zake. 28Amin, nawaambia, dhambi zote na makufuru yote ya wanadamu watasamehewa. 29Lakini yeyote anayemkufuru Roho Mtakatifu hatasamehewa kamwe, atakuwa na hatia ya dhambi ya milele.” 30Yesu alisema hivi kwa sababu walikuwa wanasema, “Ana pepo mchafu.”
Copyright information for
SwhNeno